Quotessence
Home / Topics / Malaika Quotes

Malaika Quotes

Browse 10 quotes about Malaika.

Malaika Quotes

“Binti yako mwenye umri wa miaka kumi na nne kwa mfano, anaomba umnunulie gari kama ulivyofanya kwa kaka yake mwenye umri wa miaka kumi na nane. Mara ya kwanza unamwambia utamnunulia atakapofikisha umri wa miaka kumi na nane kama ulivyofanya kwa kaka yake. Lakini baada ya wiki moja binti yako anakuomba tena kitu kilekile, yaani gari. Utajisikiaje? Utakereka, sivyo? Jinsi utakavyokereka binti yako kukuomba kitu ambacho tayari ameshakuomba, ndivyo Mungu anavyokereka sisi kumwomba vitu ambavyo tayari tumeshamwomba. Ukiomba kitu kwa mara ya kwanza Mungu amekusikia, tayari ameshaandaa malaika wa kukuletea jibu. Unachotakiwa kufanya, baada ya kuomba, shukuru mpaka jibu lako litakapofika. Mungu huthamini zaidi maombi ya kushukuru kuliko maombi ya kuomba. Binti yako anachotakiwa kufanya baada ya kukuomba gari ni kukushukuru mpaka gari yake itakapofika, si kukuomba mpaka gari yake itakapofika.”

“Mungu akikubariki kipaji chako watu watasema ni laana. Maisha yako ni sawa na mto. Unakoelekea ni baharini. Lakini sasa umefika kwenye mlango wa bahari. Unahangaika upite wapi kufika baharini, ambapo utaogelea kwa kadiri utakavyoweza. Utakapofika baharini, watu, badala ya kusema umebarikiwa, watasema umelaaniwa, badala ya kukuita malaika, watakuita shetani. Mafanikio hayapimwi kwa pesa au mali kiasi gani unayo, mafanikio yanapimwa kwa amani ya moyo au maisha ya watu kiasi gani umeboresha.”

“Shetani anaogopa viumbe saba tu hapa duniani na huko mbinguni ukimwondoa Mungu, ambaye anaogopwa na kila kiumbe: Malaika Mikaeli, Malaika Gabrieli, Malaika Rafaeli, Malaika Urieli, Malaika Selafieli, Malaika Ragueli, na Malaika Barakieli, ambao ni malaika wakuu; na tukio ambalo Shetani analiogopa zaidi ni tukio la kurudi kwa Yesu kwa mara ya pili ambalo limekaribia sana, na atafanya kila atakachoweza kabla ya tukio hilo kuchukua roho zetu. Lengo la Shetani ni kuua kila mtu duniani kumkomoa Mungu na malaika wakuu na kutupeleka kuzimu. Lakini atashindwa kwa jina la Yesu.”

“Shetani alikuwa kiumbe mzuri kuliko wote mbinguni na ulimwenguni. Mungu alimpendelea. Alikuwa mzuri kuliko malaika wote na alikuwa na nguvu kuliko kiumbe mwingine yoyote yule aliyeumbwa na Mungu, akiwemo binadamu. Lakini alipotupwa kutoka mbinguni kuja duniani kama Adamu na Hawa walivyotupwa kutoka bustanini kuja duniani, Shetani alipoteza sifa yake. Alipoteza sifa yake kwa sababu ya dhambi aliyoitenda, dhambi ya kiburi, na kwa sababu ya kuwa mbali na utukufu wa mbinguni. Badala ya kuwa kiumbe mzuri kuliko wote, Shetani akawa kiumbe mbaya kuliko wote. Mungu akaahidi kutokumsamehe, kwa sababu yeye ndiye kiumbe wa kwanza kutenda dhambi mbinguni na ulimwenguni, kwani hakushawishiwa na mtu kumuasi Mungu.”

“Shetani alikuwa malaika aliyeumbwa na Mungu lakini baadaye akamwonea Mungu wivu, wivu wa madaraka, hivyo Mungu akamtupa duniani kwa sababu ya kupingana na utawala wake mtakatifu. Duniani Shetani akamtumia nyoka kama mdakale kumdanganya Hawa. Hawa na Adamu wakamsikiliza Shetani badala ya kumsikiliza Mungu, nao wakalaaniwa. Shetani akajidai kuwa alikuwa na uwezo wa kufanya uzao wote wa Adamu na Hawa uwe mbali na Mungu, hivyo Mungu akampa muda wa kujaribu na kuthibitisha madai yake, lakini Shetani mpaka leo bado hajafanikiwa. Wakiitawala dunia leo kwa udanganyifu wa hali ya juu, pamoja naye, ni baadhi ya malaika ambao Shetani alifanikiwa kuwalaghai huko mbinguni. Mungu akawalaani pia na kuwatupa huku duniani, ambako Shetani alipapenda zaidi.”