Quotessence
Home / Authors / Enock Maregesi

Enock Maregesi Quotes

Author

Filter quotes by topic

Famous Enock Maregesi Quotes

“Mitume wa Yesu Kristo wakati wanahubiri injili hawakuwa na Roho Mtakatifu, walikuwa hata bado hawajaongoka, lakini walikuwa na idhini maalumu kutoka kwa Mungu ya kuhubiri Neno la Mungu. Neno la Mungu halihubiriwi kwa nguvu zetu sisi wenyewe bali linahubiriwa kwa nguvu za Mungu kutokana na utii kwa uongozi wake.”

“Irani itakapoipiga Israeli, kama ambavyo imeshaahidi, Israeli itajibu mapigo. Kwa vile Israeli ina nguvu zaidi kuliko Irani, itaipiga Irani kwa silaha za kawaida. Itaipiga hata kwa silaha za kinyukilia pia. Kutunisha misuli, Irani itaomba msaada wa kijeshi kutoka katika nchi za Kiarabu; ambazo zitakubali kuingilia kati na kuisaidia Irani. Kwa silaha za kawaida, bado nchi zote za Kiarabu zitakazokubali kuisaidia Irani hazitakuwa na uwezo wa kuishinda Israeli. Kuishinda itabidi zitumie silaha za kinyukilia. Silaha za kinyukilia zitakapoanza kutumika, Marekani itaingilia kati kuisaidia Israeli. Marekani itakapoingilia kati kuisaidia Israeli, Urusi itaingilia kati kuisaidia Irani. Ufaransa, Uingereza na Ujerumani zitaingilia kati kuisaidia Israeli; huku China ikiingilia kati kuisaidia Irani. Hapo Vita Kuu ya Tatu ya Dunia itaanzishwa rasmi. Katika vita hiyo ya kinyukilia na mbaya kuliko vita zote zilizowahi kupiganwa, Israeli itashinda vita na itaanzisha utawala wa Mpinga Kristo duniani kote. Kutakuwa na dini moja. Kutakuwa na serikali moja. Kutakuwa na sarafu moja. Watu watapungua hadi kufikia milioni 500, kama ilivyokuwa mwaka 1650, asilimia 7 ya idadi ya watu wote ya leo.”

“Kila binadamu ana nguvu ya ziada katika mwili wake ijulikanayo kitaalamu kama ATP. ATP (‘Adenosine Triphosphate’) ni molekuli ndogo zaidi iliyoko ndani ya seli ambayo kazi yake ni kutengeneza nguvu ya ziada kwa ajili ya seli, na kwa ajili ya mwili mzima kwa jumla, pale mwili unapoonekana kukata tamaa au kuishiwa na nguvu kabisa. Ni kama jenereta ya umeme kwa ajili ya seli, inayofanya kazi pale umeme wa kawaida unapokatika.”

“Marafiki zako wa mwanzo ambao bado ni marafiki zako mpaka sasa ni wazuri kuliko wote kutokana na sababu mbalimbali: Wamekuwepo pamoja nawe katika shida na raha; wanakujua vizuri unapokuwa na furaha, na wanakujua vizuri unapokuwa na huzuni; mmezoeana kwa miaka mingi na wanaujua hata utani wako wa ndani; wanajua nini unapendelea zaidi na nini hupendelei zaidi, na wanazijua sifa zako za ushupavu na sifa zako za udhaifu. Hata hivyo, katika maisha yetu, tunahitaji marafiki wa aina zote mbili kurahisisha maisha. Marafiki wapya hutuongezea viungo muhimu katika maisha yetu wakati marafiki wa mwanzo ni nguzo au miamba imara ya maisha yetu, na ndiyo watu hasa watakaotusaidia katika shida na raha! Usiwapoteze au usiwaache marafiki zako wa mwanzo lakini jenga mahusiano mapya. Marafiki zako wa mwanzo ni dhahabu, wa sasa ni fedha.”

“Sikujui. Lakini naamini hungependa kuishi maisha yako hapa duniani bila kuacha urithi au kumbukumbu ya aina yoyote katika jamii. Zifuatazo ni ngazi tano muhimu zitakazofanya uache dunia katika hali nzuri kuliko ulivyoikuta: Tambua vitu vya muhimu katika maisha yako ijapokuwa unaweza kuacha alama katika dunia bila kujitambua baada ya kuondoka; Tumia kipaji ulichopewa na Mungu; Fanya kazi kwa bidii na maarifa; Shindana na wenzako kuwa juu zaidi katika tasnia uliyojichagulia; Kuwa makini na kila kitu unachofanya kwa maana ubongo ni kitu cha ajabu, ubongo una uwezo wa kukupotosha.”

“Ukitambua vitu vya muhimu katika maisha yako hapa duniani na kuvipa kipaumbele cha kwanza, ukatumia kipaji ulichopewa na Mungu na ukafanya kazi kwa bidii na maarifa, halafu ukashindana na wenzako kuwa juu zaidi katika tasnia uliyojichagulia, ukafanya kila kitu kwa makini ukihofia maamuzi ya ubongo wako, utaacha urithi kwa faida ya vizazi vijavyo. Kuwa na akili, kuwa na uwezo wa kujiwekea malengo, kuwa mchapakazi hodari. Namna hiyo, hakuna kitakachoweza kushindikana.”

“Radia Hosni alikuwa na bahati kuliko watu wote duniani. Frederik Mogens alipofika katika helikopta na kukuta Murphy na Yehuda wakihangaika kuutafuta mwili wa Radia, hakushangazwa na walichomwambia. Kwa sababu alijua nini kilitokea. Radia alikutwa akipumua kwa mbali. Hivyo, Debbie na marubani walimchukua na kumpeleka Mexico City haraka ilivyowezekana. Black Hawk waliyokuwa wakiishangaa ilikuwa ya DEA. Lakini si ile waliyokwenda nayo Oaxaca. Ilikuwa nyingine ya DEA, iliyotumwa na Randall Ortega kuwachukua Vijana wa Tume na kuwapeleka Mexico City haraka ilivyowezekana. Black Hawk waliyokwenda nayo Oaxaca ndiyo iliyomchukua Radia na Debbie na kuwapeleka Altamirano (hospitali ya tume) mjini Mexico City. Mogens angekwenda pia na akina Debbie; lakini alibaki kwa ajili ya kumlinda El Tigre, na mizigo yake, na baadhi ya makamanda wake wachache. El Tigre angeweza kutoroka kama angebaki na polisi peke yao, na Mogens hakutaka kufanya makosa.”

“Watakatifu wote watanyanyuliwa na wataondoka pamoja na Yesu kuelekea mbinguni, kwa ajili ya ziara ya miaka 1000 katika ulimwengu wa roho; kuanzia dunia ya kwanza ya ulimwengu huo iitwayo Asiyah hadi ya mwisho iitwayo Adam Kadmon, katika mji mpya wa Yerusalemu. Baada ya milenia, kipindi hicho huku duniani Ibilisi akiwa kifungoni na malaika wake, binadamu wote wenye dhambi wakiwa wamekufa, Yesu na watakatifu wote atarudi kwa ajili ya ufufuo wa pili; na kama mfalme wa ulimwengu wote milele.”

“Mungu hatakubali kuwa na mtu katika ufalme wake ambaye hatakubali kutawaliwa naye. Usikubali kutawaliwa na Ibilisi, kubali kutawaliwa na Mungu. Ni jukumu letu kuanza kuishi sasa kama vile tutakavyoishi mbinguni. Shetani anataka uwe na hekima ya duniani ili akupumbaze. Lakini hofu ya Mungu ndiyo msingi wa hekima ya kweli. Ukitaka asikupumbaze, pokea Roho ya Mungu kwa kubatizwa. Ukiipokea Roho ya Mungu utajua mambo ya Mungu, ambayo dunia haiwezi kujua.”

“Yesu alipokuwa msalabani watu wengi walimzunguka. Askari wa Kirumi aliyekuwa na chongo, na mkuki, alikuwa na jukumu la kumtesa Yesu hadi kufa kwa amri ya Pilato. Yesu alipolia kwa sauti kuu, “Eloi, Eloi, lama sabakthani?”, yule askari alikurupuka na kumwendea Yesu. Lakini Yesu alishakata roho. Kuthibitisha kama Yesu alishakata roho, askari alimchoma Yesu mkuki kwenye mbavu kwa nguvu zake zote. Mkuki huo ukamtoboa Yesu hadi upande wa pili, ukatoboa hata moyo wake. Askari alipochomoa mkuki, damu na maji viliruka na kupiga jicho lake bovu. Papo hapo askari akapona na kuona vizuri. Alipoona kweli amepona na kuona vizuri, askari alipiga kelele, alipiga magoti na kuomba Mungu amsamehe dhambi zake. Msamaha una nguvu kuliko dhambi. Askari huyo atakwenda mbinguni. Haijalishi umechukia watu kiasi gani. Haijalishi umetesa watu kiasi gani. Haijalishi umeua watu kiasi gani. Haijalishi umetenda dhambi kiasi gani. Mungu anachotaka kutoka kwako, tubu.”

“Shetani anaogopa viumbe saba tu hapa duniani na huko mbinguni ukimwondoa Mungu, ambaye anaogopwa na kila kiumbe: Malaika Mikaeli, Malaika Gabrieli, Malaika Rafaeli, Malaika Urieli, Malaika Selafieli, Malaika Ragueli, na Malaika Barakieli, ambao ni malaika wakuu; na tukio ambalo Shetani analiogopa zaidi ni tukio la kurudi kwa Yesu kwa mara ya pili ambalo limekaribia sana, na atafanya kila atakachoweza kabla ya tukio hilo kuchukua roho zetu. Lengo la Shetani ni kuua kila mtu duniani kumkomoa Mungu na malaika wakuu na kutupeleka kuzimu. Lakini atashindwa kwa jina la Yesu.”

“Shetani alikuwa kiumbe mzuri kuliko wote mbinguni na ulimwenguni. Mungu alimpendelea. Alikuwa mzuri kuliko malaika wote na alikuwa na nguvu kuliko kiumbe mwingine yoyote yule aliyeumbwa na Mungu, akiwemo binadamu. Lakini alipotupwa kutoka mbinguni kuja duniani kama Adamu na Hawa walivyotupwa kutoka bustanini kuja duniani, Shetani alipoteza sifa yake. Alipoteza sifa yake kwa sababu ya dhambi aliyoitenda, dhambi ya kiburi, na kwa sababu ya kuwa mbali na utukufu wa mbinguni. Badala ya kuwa kiumbe mzuri kuliko wote, Shetani akawa kiumbe mbaya kuliko wote. Mungu akaahidi kutokumsamehe, kwa sababu yeye ndiye kiumbe wa kwanza kutenda dhambi mbinguni na ulimwenguni, kwani hakushawishiwa na mtu kumuasi Mungu.”

“Utajiri wa mbinguni ni wa milele na mungu wake ni Yehova. Utajiri wa duniani ni wa muda na mungu wake ni Mammon. Mammon, ambaye hata Yesu alimtaja katika Injili ya Mathayo 6 na katika Injili ya Luka 16, ni mungu wa uchoyo na utajiri wa dunia hii. Mammon kazi yake ni kufanya watu waliokufa kifedha na walio hai kifedha kuwa maskini wa milele ahera. Yesu Kristo alikuwa maskini, ili tuwe matajiri kupitia umaskini wake, lakini kwa sababu alikuwa na imani ya Mungu katika moyo wake alikuwa tajiri. Hivyo unaweza kuwa na utajiri wa mbinguni hapa duniani, ukiikaribisha amani ya Mungu katika moyo wako.”